Breaking News

MAKTABA YA WATOTO HOSPITALI YA MKOA WA MWANZA NI KIVUTIO KWA WAKUBWA NA WATOTO

                                                  Na Tonny Alphonce, Mwanza

Maktaba Ya Watoto ni chumba maalumu cha watoto kucheza kikiwa kimepambwa na vifaa mbalimbali vya kuchezea watoto huku kuta zake zikiwa zimepambwa na michoro ya herufi mbalimbali.


Chumba hiki ukiingia kwa mara ya kwanza unaweza kudhani upo shuleni katika darasa la kisasa la  wanafunzi wa madarasa ya awali kwa kuwa chumba kinaongea.

Maktaba hii ipo mkoani Mwanza katika Hospitali ya Mkoa ya Mwanza (Sekou Toure)na inaelezwa kuwa kwa Tanzania Maktaba za watoto zipo mbili tu nchi nzima.

Kwanini maktaba hii ya watoto imewekwa hospitalini?

Afisa Ustawi wa jamii mkoa wa Mwanza Faithmary Lukindo anasema vyumba hivi ni muhimu kwa kuwa vinasaidia watoto kupata nafuu ya magonjwa haraka lakini pia watoto kupata uchangamshi na kuweza kuwasiliana na wenzao kupitia michezo inayofundishwa katika Maktaba hizo.

Afisa Ustawi wa jamii mkoa wa Mwanza Faithmary Lukindo akizungumzia namna Maktaba ya Watoto inavyofanyakazi

Faithmary amesema waliamua kuanzisha maktaba hii hospitalini ili kuwasaidia watoto ambao wamelazwa waweze kupata nafasi ya kujifunza kupitia Maktaba ya Watoto ambayo kiuhalisia inawasaidia pia kupunguza maumivu ya ugonjwa wanaopitia kwa kipindi hicho.

“Mtoto anapoendelea kukua magonjwa ni sehemu katika ukuaji wake lakini hata anapokuwa ameugua ukuaji hausimami hatua za ukuaji zinaendelea kama kawaida na ubongo unaendelea kukua kama kawaida kwa hiyo maktaba hii inamsaidia mtoto kupata fursa ya kujifunza pale anapopata nafuu kidogo wakati akiendelea na matibabu”.alisema Faithmary

Kwa upande wake Teddy John afisa ustawi katika hospitali ya Sekou toure  kitengo cha ustawi wa jamii amesema maktaba hii wa watoto inawasaidia sana watoto wanaolazwa kwa muda mrefu kupata nafasi ya kujifunza huku wakiendelea na matibabu.

Teddy John afisa ustawi katika hospitali ya Sekou Toure  kitengo cha ustawi wa jamii akizungumzia faida wanayopata watoto katika chumba cha Maktaba ya Watoto

Teddy amesema kuna watoto wanalazwa miezi miwili au zaidi hii husababisha mtoto kupitwa na masomo lakini kupitia maktaba hii inawasaidia watoto kuendelea kujifunza na atakapo pona anaweza kuendelea na masomo yake bila tatizo lolote.

“Kabla hatujaanzisha maktaba hii ya watoto ilikuwa mtoto anashinda wodini muda wote na ilikuwa ikisababisha watoto kukosa amani na kulia muda wote lakini baada ya kuanzisha maktaba hii ya watoto tumeona tofauti maana mtoto akiisha ingia kwenye chumba hiki anabadilika anachangamka anaanza kucheza kwa kuwa kuna vitu vingi vya michezo tumewawekea”.alisema Teddy


Pendo Jackobo kutoka idara ya watoto ambaye ndio msimamizi wa watoto hao amesema amekuwa akienda kuwachukua watoto mara baada ya daktari kupita na kuwapatia matibabu.

Pendo Jackobo kutoka idara ya watoto ambae ndiye msimamizi wa watoto katika Maktaba ya Watoto akielezea namna anavyo wahudumia watoto 

Amesema katika maktaba hiyo wapo watoto wanaojifunza kusoma na kuandika na wapo watoto ambao wao hucheza kupitia michezo mbalimbali iliyopo katika chumba hicho.

“Kwa kweli watoto hufurahia sana wanapokuwa hapa maana kuna midori kuna magari wanaendesha kiasi kwamba watoto wengine wakiishaingia  maktaba kucheza huwa hawataki kuondoka kutokana na michezo iliyopo kuwavutia”.alisema Pendo

Mmoja wa wazazi ambae amelazwa hospitalini hapo kwa zaidi ya mwezi mmoja amesema mara ya kwanza msimamizi wa Maktaba ya Watoto alipoenda kumchukua mtoto wake alikuwa na wasiwasi kuwa mtoto wake ataenda kusumbua lakini ilikuwa tofauti kabisa na alivyofikiria.

Mzazi akicheza na watoto katika Maktaba ya Watoto michezo mbalimbali

“Matroni alipokuja kumchukua mtoto mara baada ya kutibiwa na daktari nilitaka kumkatalia lakini nikashangaa nusu saa nzima kimya mtoto hajarudishwa maana namjua mtoto wangu huwa mara nyingi anapenda kuwa na mimi tu sasa nikaamua kwenda kumuona nilipoingia kwenye Maktaba hiyo ya Watoto nilishangaa ilivyo nzuri na nilishangaa kumuona mtoto wangu amechangamka anacheza utadhani haumwi”.alisema mzazi huyo

Bila shaka katika tafiti zilizopangwa kufanyika ili kusaidia mchakato wa kutengeneza taarifa ya utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Malelezi, Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto (MMMAM) kwa  kutambua ubunifu, mbinu zilizoleta matokeo chanya, vizuizi na viwezeshi utaigusa hospitali hii ya mkoa wa Mwanza (Sekou Toure) kwa ubunifu huu wa kuwa na Maktaba Ya Watoto kwaajili ya watoto wanaotibiwa katika hospitali hiyo.

No comments