Breaking News

VIFO VYA KINA MAMA WAJAWAZITO NA WATOTO BADO TATIZO MWANZA RC ATAKA KILA MMOJA AWAJIBIKE.

 Na Tonny Alphonce,Mwanza.

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhandisi Robert Gabriel amewataka wananchi na wadau wa afya kufanya mageuzi makubwa ya kimaisha na kimatibabu ili kupunguza vifo vya mama na mtoto ambavyo bado ni tatizo kubwa mkoani Mwanza.

Amesema takwimu zinaonyesha mwaka 2020 kina mama 157 walifariki dunia wakati wa kujifungua,wakati mwaka 2021 kina mama 164 walifariki dunia na mwaka 2021 watoto wachanga 669 walifariki dunia hali ambayo sio nzuri.

Kauli hiyo ameitoa wakati wa makabidhiano ya Zahanati Lumala Magharibi iliyopo wilayani Ilemela Mkoani Mwanza ambapo kitatoa huduma kwa wakazi wa kata ya Ilemela na wananchi wa kata za Jirani.

Mkuu wa Mkoa Mhandisi Gabriel akizungumza mara baada ya uzinduzi wa Zahanati ya Lumala Magharibi.

Akizungumza mara baada ya uzinduzi wa Zahanati hiyo Mhandisi Gabriel amewataka wananchi na madaktari kushirikiana pamoja hasa kwa kina mama wajawazito ili waweze kujifungua salama na kupunguza vifo vya kina mama na Watoto.

‘Ndugu zangu Mama mjamzito anatakiwa kuripoti kwenye kituo cha afya mara baada ya kugundua kuwa anaujauzito ili aweze kuandikishwa na kupimwa afya yake hii itamsaidia mama kusafiri salama  katika safari yake ya ujauzito hayo yote kwa pamoja yakifanyika yatamuhakikishia mama usalama wake pamoja na mtoto.alisema Mhandisi Gabriel.’

Mhandisi Gabriel amesema kwa upande wa serikali ya mkoa tayari hatua mbalimbali zimeisha chukuliwa ikiwemo kuhakikisha ujenzi wa vituo vya afya na Zahanati vinaendelea,Elimu ya uzazi salama imekuwa ikitolewa pamoja na kutekeleza mipango mbalimbali ya kitaifa ukiwemo mpango Jumuishi wa Taifa wa Malezi ,Makuzi na Maendeleo ya awali ya Mtoto ambao unagusia pia afya ya mama na mtoto.

Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Ilemela Hassan Masala amesema maboresho yote ya afya yanayofanywa na serikali mnufaika wa kwanza huwa ni mama na mtoto na amemshukuru Rais kwa kuendelea kutoa fedha za ujenzi wa vituo vya afya.

‘Niombe kina mama mtumie sasa Zahanati hii pale mnapopata matatizo mbalimbali ya kiafya,msikimbilie hospitali ya mkoa au Bugando kule nendeni tatizo linapokuwa kubwa tena kwa maelekezo ya madaktari wenu wa hapa nasema hivyo ili hospitali ya mkoa na Bugando wapumue huko waende wale watakaokuwa mahututi.alisema Masala’


Mkuu wa wilaya ya Ilemela Hassan Masala akizungumza katika uzinduzi wa Zahanati ya Lumala Magharibi.

Akitoa taarifa ya ujenzi wa Zahanati hiyo kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilemela Mofen Mwakatonga amesema jumla ya shilingi milioni 152 na laki 2 zimetumika kukamilisha ujenzi wa Zahanati hiyo ambayo itawasaidia wananchi wa mitaa ya Lumala,Masemele na Nyamadoke watapata huduma katika umbali mfupi na hatimaye kupunguza vifo vya mama na mtoto.

Naye mmoja wananchi waliofika katika kushuhudia makabidhiano hayo Rose Mushi amesema kuanza kufanyakazi kwa Zahanati hiyo kutawasaidia kina mama wengi wenye ujauzito na wenye Watoto wadogo kupata huduma kwa wakati.

Mwananchi Rose Mushi akizungumzia faida watakazopata mara baada ya zahanati hiyo kuanza kufanyakazi.

Rose amesema pamoja na kuanza kufanyakazi kwa Zahanati hiyo bado serikali inatakiwa kuhakikisha wahudumu wa afya wanakuwepo pamoja na kuanzisha huduma nyingine za upasuaji.

Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela imeendelea kukamilisha ujenzi  wa Zahananti mpya tatu zilizoanzishwa kwa nguvu za wananchi,ujenzi wa Zahanati ya Lumala Magharibi ulianza rasimi mwaka 2018 na kukamilika mwaka 2022.

Mpango huu wa kuboresha huduma za afya katika maeneo mbalimbali nchini unaendana na lengo la  Programu Jumuishi Malezi,Makuzi na Maendeleo ya awali ya mtoto katika kupunguza idadi kubwa ya vifo vya watoto chini ya miaka mitano.

No comments