Breaking News

WATAALAMU WA AFYA:MTOTO ALIYEKO TUMBONI HAWEZI KUPATA UVIKO 19

 

Na Tonny Alphonce,Mwanza.

Kisayansi mtoto aliyepo tumboni kwa mama hawezi kupatwa na ugonjwa wa UVIKO 19 kwa kuwa maambukizi ya ugonjwa huo yanaenea kwa njia ya hewa.

Picha ya pamoja kati ya waandishi wa habari na timu ya Mganga Mkuu Wa Dkt Thomas Rutachunzibwa .

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Utafiti Chuo Kikuu Bugando Mwanza  Dkt Benson Kidenya wakati wa mkutano wa maswali na majibu juu ya UVIKO 19 baina ya waandishi wa habari wa mkoa wa Mwanza na Ofisi ya Mganga mkuu wa mkoa wa Mwanza.

Dkt Benson Kidenya Mkurugenzi wa Utafiti Chuo Kikuu Bugando Mwanza akijibu baadhi ya maswali ya waandishi wa habari hawapo kwenye picha.

Dkt Kidenya amesema mtoto anaweza kuambukizwa ugonjwa wa UVIKO 19 mara baada ya kuzaliwa japo kuwa kisayansi watoto wachanga wamekuwa hawapatwi na ugonjwa UVIKO 19 japo wanaweza kuwa na virusi vya UVIKO 19.

Amesema kuhusu chanjo kwa kina mama wajawazito bado serikali inaendelea  kufanya utafiti kujua ni wakati gani mzuri kwa mama mjamzito kupatiwa chanjo.

Dkt Kidenya amesema kwa kawaida mama mjamzito kinga zake huwa zinashuka hivyo ni vema akapatiwa chanjo kwa katika kipindi hicho kwa kuwa anaweza kushambuliwa na magonjwa mbalimbali ikiwemo ugonjwa wa UVIKO 19.

”Utafiti wa awali ulipendekeza mama mjamzito ni vema akachanjwa wakati mimba yake ikiwa imesogea kidogo kwa sababu katika kipindi cha mwanzo cha ujauzito ndio mtoto anaumbwa sio vema mama kutumia dawa nyingi,hivyo tunasubiri maelekezo ya serikali katika hili”alisema Dkt Kidenya.

Kwa upande wake Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mwanza,Dkt Thomas Rutachunzibwa amewataka kina mama wajawazito wasiwe na haraka ya kutaka kupatiwa chanjo ya UVIKO 19 kwa kuwa serikali itatoa mwongozo juu ya wajawazito na kina mama wanaonyoshesha kipindi gani wapatiwe chanjo hizo.

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mwanza,Dkt Thomas Rutachunzibwa akijibu baadhi ya maswali juu ya chanjo ya UVIKO 19.

Dkt Rutachunzibwa amesema lengo la serikali ni zuri kwa kuwa kipindi cha miezi mitatu ya ujauzito hiki ndio kipindi mtoto anaumbika hivyo sio vizuri mama kupatiwa dawa nyingi kwa sababu mtoto anaweza kuzaliwa akiwa na kasoro za kimaumbile.

“Watoto wengi wanaozaliwa na matatizo kama ya mgongo wazi au kichwa kikubwa sababu huwa ni mama kutumia dawa nyingi wakati wa ujauzito wake ndio maana miezi hii ya awali ya ujauzito hatutaki kumpatia mama mjamzito dawa nyingi”alisema Dkt Rutchunzibwa.

Akizungumzia zoezi la chanjo ya UVIKO 19 linavyoendelea mkoani Mwanza Dkt amesema wananchi wanahamasika na hadi hivi sasa watu zaidi ya elfu 28 wamepata chanjo na hakuna madhara yoyote yanayotokana na chanjo yameripotiwa.

Dkt Rutachunzibwa amesema mwako mkubwa wa wananchi kuchanja kwa mkoa wa Mwanza ni kutoka vijijini hasa katika wilaya za Kwimba,Misungwi na Magu na kuwataka waandishi kuwahimiza wananchi wanaoishi mijini kwenda kuchanja.

No comments